Breaking News

Your Ad Spot

Mar 10, 2015

UDHIBITI WA BIDHA ZA CHAKULA , DAWA, VIPODOZI NA VIFAA TIBA KATIKA VITUO NYA FORODHA

Kaimu Meneja Mawasiliano na Uhusiano wa Mamlaka ya Chakula na Dawa (TFDA), Gaudensia Simwanza, akizungumza na waandishi wa habari, Dar es Salaam leo, wakati alipokuwa akielezea kuhusu kazi na majukumu ya taasisi hiyo kwa jamii, Pia udhibiti wa bidhaa za chakula, Dawa, Vipodozi na Vifaa tiba katika Vituo vya Forodha. Kulia ni Ofisa Uelimishaji Jamii wa TFDA, James Ndege. (Picha zote na Kassim Mbarouk-www.bayana.blogspot.com)
Kaimu Meneja Mawasiliano na Uhusiano wa Mamlaka ya Chakula na Dawa (TFDA), Gaudensia Simwanza, akizungumza na waandishi wa habari, Dar es Salaam leo. 
Baadhi ya waandishi wa habari wakifuatilia maelezo yaliyokuwa yakitolewa na Kaimu Meneja Mawasiliano na Uhusiano wa Mamlaka ya Chakula na Dawa (TFDA), Gaudensia Simwanza, wakati wa mkutano huo, Dar es Salaam leo. 
Waandishi wa habari
Napenda kwa heshima na taadhima kutumia fursa hii kwa niaba ya Menejimenti ya TFDA na wafanyakazi wote kwa ujumla kuwakaribisha katika mkutano huu.  TFDA ni taasisi ya Serikali iliyopo chini ya Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii iliyoundwa chini ya sheria namba 1 ya Chakula, Dawa na Vipodozi  Sura 219 kwa lengo la kudhibiti ubora na usalama wa chakula, dawa, vipodozi na vifaa tiba ili kulinda afya za wananchi.
Ndugu wanahabari,
Pamoja na kazi nyingine za kiudhibiti, TFDA imeweka taratibu na kanuni katika kusajili, kuingiza na kutoa bidhaa hapa nchini. Leo nitazungumzia kuhusu mkakati wa wa TFDA katika udhibiti wa bidhaa za chakula, dawa, vipodozi na Vifaa tiba katika vituo vya forodha kabla ya kuruhusiwa kuingia katika soko kwa bidhaa zinazotoka nje ya nchi au kusafirishwa nje ya nchi kwa lengo la kujiridhisha na usalama, ubora na ufanisi wake.  
Ndugu wanahabari,
Vituo vya forodha ni vituo rasmi vya mipakani vinavyotambulika kisheria kwa ajili ya kuruhusu uingizaji na utoaji wa bidhaa ndani na nje ya nchi. Taasisi tofauti za usimamizi wa sheria zinakuwepo kwenye vituo vya forordha kwa lengo la kusimamia sheria na taratibu zinazohusiana na udhibiti wa bidhaa mbalimbali. Vituo hivyo vya forodha ni kama vile bandari, viwanja vya ndege na bandari kavu kwa maana ya mpaka wa nchi na nchi.

TFDA imeweka mifumo ya udhibiti wa uingizaji wa bidhaa za chakula, dawa, vipodozi na vifaa tiba katika vituo vya forodha ambapo kwa upande wa chakula vituo vya forodha vinavyoruhusiwa kupitisha chakula ni  vituo 32 na kwa upande wa dawa ni vituo 10. Hii ina maana kuwa mwingizaji wa bidhaa kutoka nje ya nchi ni lazima aainishe kituo cha forodha ambacho bidhaa zake zitapita wakati wa kuingiza nchini ambako kuna wakaguzi wa bidhaa hizo. (Orodha ya vituo imeainishwa hapa chini)
Vituo vya forodha kwa ajili ya kuingiza dawa
S/N
Jina la Kituo cha Forodha
S/N
Jina la Kituo cha Forodha
1.
Namanga
6.
Kasumulu
2.
Sirari
7.
Dar es Salaam Airport
3.
Tunduma
8.
Kilimanjaro Airport
4.
Holili
9.
Dar es Salaam Seaport
5.
Horohoro
10.
Tanga Seaport

Vituo vya Forodha kwa ajili ya kuingiza vyakula
S/N.
Jina la Kituo cha Forodha
S/N.
Jina la Kituo cha Forodha
1.
Namanga
17.
Dar es Salaam Airport
2.
Sirari
18.
Kilimanjaro Airport
3.
Tunduma
19.
Kipili Seaport
4.
Holili
20.
Lindi Seaport
5.
Horohoro
21.
Mtwara Seaport
6.
Tarakea
22.
Mbamba Bay Seaport
7.
Rusumo
23.
Mwanza Seaport
8.
Mutukula/Kyaka
24.
Musoma Seaport
9.
Isaka
25.
Bagamoyo Seaport
10.
Kabanga
26.
Bukoba Seaport
11.
Kasumulu
27.
Dar es Salaam Seaport
12.
Mabamba
28.
Tanga Seaport
13.
Manyovu
29.
Itungi Seaport
14.
Mafia
30.
Kasesya Seaport
15.
Mwanza Airport
31.
Kemondo Seaport

Ndugu wanahabari,
TFDA inadhibiti uingizaji wa bidhaa za chakula, dawa, vipodozi, na vifaa tiba kwa lengo la kulinda afya za mlaji au mtumiaji dhidi ya madhara yatokanayo na bidhaa zisizofaa kwa matumizi ya binadamu. Pia, kuhakikisha kuwa nchi yetu haifanywi kuwa jalala la bidhaa mbovu, duni na bandia kutoka nje ya nchi na kuepusha usambazaji na uuzwaji wa dawa, chakula, vipodozi na Vifaa tiba vyenye lebo zinazopotosha.  Aidha, kwa kufanya hivyo tunawadhibiti wafanyabiashara wasio waaminifu ambao kwa tamaa ya pesa wanaweza kusababisha uingizaji wa bidhaa zisizo kidhi vowango vya salama na ubora nchini.
Mfanyabiashara akitaka kuingiza bidhaa nchini kwanza kabisa anapaswa kupata mwongozo na kanuni ili kufahamu taratibu za usajili na uingizaji wa chakula, dawa, vipodozi na vifaa tiba nchini.
Ndugu wanahabari,
          Kwenye vituo vya forodha kuna wataalam wanaosimamia sheria mbalimbali za nchi ambapo TFDA ni miongoni mwa taasisi zenye uwakilishi katika vituo hivyo. TFDA imeweka wakaguzi katika vituo vya forodha ambapo ukaguzi na usimamizi wa sheria umeimarishwa kwa kushirikiana na taasisi nyingine kama vile TRA, Jeshi la Polisi, TBS n.k.

Wakaguzi hao wamekuwa wakifanya kazi ya kuhakikisha bidhaa zinazorohusiwa kuingia nchini ni zenye usalama, ubora na ufanisi kwa mujibu wa vibali vilivyoombewa. Kwa mfano, mwaka 2013/14, Mamlaka ilipokea jumla ya maombi 11,887 ya vibali vya kuingiza nchini chakula, dawa, vipodozi na vifaa tiba, ambapo kati ya hayo Maombi 10,341 (87%) yalitimiza vigezo  na vibali kutolewa. Maombi 1,546(13%) yalikataliwa kutokana na kutokukidhi matakwa ya sheria na hivyo bidhaa husika kutoruhusiwa kuingizwa nchini. Vile vile, maombi 727 ya vibali vya kusafirisha nje ya nchi chakula, dawa, vipodozi na vifaa tiba yalipokelewa. Kati ya hayo, maombi 312 yaliidhinishwa na maombi 415 yalikuwa na hoja mbalimbali kwa sababu ya kutokidhi matakwa ya sheria. Aidha, ukaguzi wa bidhaa katika vituo vya forodha umeendelea kuimarika na hivyo kusaidia kudhibiti uingizaji wa bidhaa duni na bandia nchini.
Ndugu wanahabari,
Wakaguzi wa TFDA katika vituo vya forodha wana jukumu la kuhakikisha kwamba kila bidhaa inayoingizwa nchini ina kibali cha TFDA.  Kwa hivyo wakaguzi hawa hulinganisha bidhaa zilizoonyeshwa kwenye kibali husika na bidhaa halisi iliyoingizwa.  Pia, bidhaa husika hukaguliwa kuona kama ipo katika hali nzuri ya usalama na ubora. Aidha, maabara ndogo zinazohamishika (Mini lab Kit) hutumiwa na wakaguzi kuchunguza sampuli za mizigo ya dawa kabla ya kuruhusiwa kuingia nchini na pia wanatumia maabara maalum (Stelite Laboratories) kuchunguza madini joto katika chumvi kwa upande wa chakula. Pale ukaguzi na matokeo ya uchunguzi wa sampuli za bidhaa katika kituo cha forodha unapoonyesha wasi wasi juu ya usalama na ubora wa bidhaa husika, sampuli huchukuliwa kwa ajili ya uchunguzi zaidi katika Maabara kuu ya TFDA iliyoko Makao Makuu ya TFDA Dar es Salaam.

Iwapo baada ya uchunguzi wa kimaabara, bidhaa itaonekana haikidhi viwango vilivyowekwa, amri inatolewa kurudisha mzigo wote ulikotoka kwa gharama ya muingizaji.  Uamuzi huu wa kurudisha bidhaa mbovu zilikotoka unaweza kutolewa hata bila kufanya uchunguzi wa maabara kama ubovu huo upo wazi na unaonekana kwa macho.  Kwa mfano, kama mahindi yameoza au kushambuliwa na wadudu hakuna haja ya kufanya uchunguzi wa kimaabara kabla ya kutoa amri ya kuyarudisha yalikotoka. Pia bidhaa zisizofaa zinaweza kuharibiwa hapa nchini kwa gharama za mwagizaji. Vilevile, bidhaa ambayo tarehe ya mwisho ya matumizi yake (expiry date) imekaribia kumalizika haiwezi kuruhusiwa kuingia nchini.  Kwa mfano sheria inataka bidhaa kuwa na muda wa matumizi unaozidi miezi sita kabla ya kuruhusiwa kuingia nchini.  Upungufu mwingine ni kama bidhaa haijasajiliwa au mwingizaji hajapata kibali cha kuingiza bidhaa husika au isiyokuwa na maelezo sahihi kwenye lebo.  Pia, bidhaa zilizopigwa marufuku hazitaruhusiwa kuingia nchini.

Ndugu wanahabari,
Baadhi ya changamoto tunazokabiliana nazo ni kama zifuatazo:-
·      Uwepo wa mifumo tofauti ya kiudhibiti kwa nchi za jirani;
·      Bidhaa kupitia katika vituo visivyotambulika maarufu kama “njia za panya”;
·      Uingizwaji wa bidhaa bandia na duni zilizotengenezwa kwa kutumia teknolojia ya hali ya juu kiasi cha kutoweza kutambulika kirahisi wakati wa ukaguzi mipakani;
·      Utandawazi na soko huria ambalo limesababisha kuongezeka kwa biashara na ushiriki wa wafanyabiashara wengi wenye mbinu za kukwepa taratibu za udhibiti wa bidhaa;
·      Uelewa mdogo wa baadhi ya wafanyabiashara na walaji juu ya dhana nzima ya usalama na ubora wa chakula.

Ndugu wanahabari,
Katika kukabiliana na changamoto hizi, Mamlaka imeendelea kuwatumia  na kuwajengea uwezo wakaguzi wa Halmashauri, kushiriki kikamilifu katika majadiliano ya kuwianisha mifumo ya udhibiti wa bidhaa hasa katika Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) na SADC, kubuni mbinu za kupambana na matumizi mabaya ya teknolojia na kuendelea kuelimisha jamii juu ya matumizi sahihi ya bidhaa zinazodhibitiwa na Mamlaka.  

Ndugu wanahabari,
Kwa kuhitimisha, naomba kwa niaba ya TFDA nitoe shukran za dhati kwenu waandishi wa habari kwa ushirikiano ambao mmekuwa mkiuonesha katika kutoa taarifa za kiudhibiti pale inapotokea pamoja na kuelimisha jamii. Rai yetu kwenu ni kuendelea kutumia kalamu zenu katika kuwaondolea hofu wananchi kuhusu usalama na ubora wa bidhaa za chakula, dawa, vipodozi na vifaa tiba vilivyopo katika soko kutokana na mifumo thabiti iliyowekwa na TFDA. Aidha, niwaombe msisitize kuwabaini na kutoa taarifa kwa TFDA na Umma kuhusu vitendo vya ukiukaji sheria na hivyo kuhatarisha maisha ya jamii.

Aidha, tunawaomba wananchi kuendelea kutoa ushirikiano katika kuwafichua wafanyabiashara watakaovunja sheria kwa kuingiza nchini bidhaa za chakula, dawa na vifaa tiba bila kufuata taratibu ikiwa ni pamoja na kutumia njia za panya kwa kutoa taarifa katika ofisi za TFDA Makao Makuu zilizipo Extenal Mabibo na ofisi za Kanda zilizopo katika mikoa ya Mwanza, Arusha, Mbeya, Dodoma, Mtwara na Dar es Salaam pamoja na Ofisi za Waganga wakuu wa Mikoa na Wilaya au kituo chochote cha polisi kilicho jirani naye.

Asanteni kwa kunisikiliza!

No comments:

Post a Comment

Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages