Breaking News

Your Ad Spot

Nov 2, 2016

MABADILIKO YA BARAZA LA MAWAZIRI EDHIOPIA

Waziri Mkuu wa Ethiopia amelifanyia marekebisho baraza lake la mawaziri katika jaribio la kutaka kuzima maandamano na malalamiko ya watu wa makabila ya Oromo na Amhara wanaoituhumu serikali, inayodhibitiwa na kabila la Tigray, kwamba inawabagua .
Waziri Mkuu Hailemariam Desalegn amechukua hatua hiyo wiki tatu baada ya kutangaza hali ya hatari nchini humo ambapo wakati huo aliahidi kulifanyia mabadiliko baraza lake la mawaziri.
Katika mabadiliko hayo, Desalegn amewateua wanasiasa wawili kutoka kabila la Oromo kuchukua wizara mbili muhimu. Watu wa kabila hilo wamekuwa mstari wa mbele katika maandamano na malalamiko ya miezi kadhaa sasa dhidi ya serikali ya Addis Ababa ambayo yamepelekea kuuawa mamia ya watu. Waandamanaji pia wanataka kuachiliwa huru wafungwa wa kisiasa ambao wanashikiliwa kwa kushiriki katika maandamano ya miezi kadhaa ambayo hadi sasa yamesababisha karibu watu 500 wapoteza maisha huku wapinzani wakisema idadi hiyo ni kubwa zaidi kuliko iliyotnagazwa.
Hatua ya Waziri Mkuu Desalegn ya kuwapa watu wa kabila la Oromo nafasi mbili muhimu katika baraza la mawasiri imetajwa kuwa jibu muafaka kwa matakwa ya Waoromo.  Workneh Gebeyehu wa kabila la Oromo sasa ni waziri wa mambo ya nje, na Negeri Lencho ni waziri wa habari.
Katika mabadiliko mapya ya baraza la mawaziri ni mawaziri tisa tu wa baraza lililopita la mawaziri 30 waliosalia katika nafasi zao. Kati ya walioachwa bila kuguswa ni mawaziri wa ulinzi, usalama wa mataifa na naibu waziri mkuu katika baraza la mawaziri. Jambo hilo linaonyesha wazi kuwa, nafasi muhimu na nyeti zingali zinashikiliwa na kabila la wachache la Tigray.
Mawaziri wapya kutoka kabila la Oromo ni wanachama wa chama tawala cha People’s Revolutionary Democratic Front, (PRDF) ambacho kimetawala Ethiopia kwa muda wa miaka 25. Aidha aghalabu ya wabunge ni ni wanachama wa chama hicho na kwa msingi huo bunge hilo limeidhinisha baraza jipya la mawaziri bila mjadala.
Waziri Mkuu Desalegn hata hivyo amesisitiza kuwa, katika mabadiliko aliyofanyia baraza la mawaziri, kigezo kikuu hakikuwa utiifu kwa chama tawala bali amezingatia zaidi utaalamu wa mawaziri walioteuliwa. Pamoja na hayo, weledi wa mambo wanaamini kuwa, hata kwa kuteuliwa mawaziri wawili kutoka kabila la Oromo, maandamano na madai ya watu wa kabila hilo hayatamalizika.
Ni wazi kuwa waandamanaji wa kabila la Oromo magharibi mwa Ethiopia na wale wa kabila la Amhara kaskazini mwa nchi hiyo hawatakubali kusitisha upinzani wao kutokana tu na mabadiliko katika baraza la mawaziri.
Waandamanaji wa kabila la Oromo nchini Ethiopia
Kwa muda wa miaka 25 sasa chama tawala cha PRDF  ambacho wafuasi wake wengi ni wa kabila la Tigray, kimeitawala Ethiopia pasina kuwepo maandamano. Kwa hivyo maandamano ya miezi michache iliyopita yamewashtua watawala wa Ethiopia ambao walidhani utawala wao hauwezi kutikisika.
Ukandamizaji wa maandamano umekuwa mbaya sana kiasi cha mashirika ya kimatiafa ya kutetea haki za binadamu kuikosoa serikali ya Addis Ababa.
Weledi wa mambo wanasema demokrasia halisi, hasa katika nchi za Afrika, inapaswa kujumuisha watu wa makabila yote makubwa na muhimu katika nchi sambamba na kuwepo uhuru wa maoni na vyombo vya habari.
Inasuburiwa kuona iwapo Waamhara na Waoromo wataafiki mabadiliko mapya katika baraza la mawaziri au wataendeleza maandamano wakitaka mabadiliko zaidi yafanyike.

No comments:

Post a Comment

Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages