Breaking News

Your Ad Spot

Nov 3, 2016

KUSHADIDI MIVUTANO KATIKA UHUSIANO WA KISIASA WA RWANDA NA BURUNDI

Hitilafu na mivutano ya kisiasa kati ya nchi za Rwanda na Burundi imepamba moto tena baada ya kuuawa raia mmoja wa Burundi katika eneo la mpaka wa nchi hizo mbili.
Maafisa wa polisi ya Burundi wanasema kuwa askari wa Rwanda wamempiga risasi na kumuua raia mmoja wa nchi hiyo wakati raia watatu walipokuwa wakivuka maji ya ziwa Rweru lililoko kwenye mpaka wa nchi hizo mbili. Raia mwingine anashikiliwa na jeshi la Rwanda. Hii ni mara ya pili kwa raia wa Burundi kupigwa risasi na kuuawa na jeshi la Rwanda katika kipindi cha mwezi mmoja uliopita.
Uhusiano wa nchi hizo mbili jirani umepooza na kuzorota tangu ulipoanza mgogoro wa ndani wa Burundi Aprili mwaka jana. Kugombea na kuchaguliwa tena Rais Pierre Nkurunziza katika uchaguzi wa mwaka jana kumeitumbukiza Burundi katika mgogoro mkubwa wa kisiasa ambao bado unatokota. Maafisa wa serikali ya Burundi wanaituhumu Rwanda kuwa inawasaidia na kuwaunga mkono waasi wanaotaka kuiondoa madarakani serikali ya Rais Nkurunziza. Wapinzani wa kiongozi huyo wanamtuhumu yeye na chama tawala kuwa walifanya mapinduzi dhidi ya katiba ya nchi hiyo na kwamba kiongozi huyo hakustahiki kugombea tena kiti cha rais baada ya kukamilisha kipindi cha pili cha uongozi wake.
Machafuko ya ndani Burundi
Tangu ulipozuka mgogoro wa kisiasa kati ya nchi hizo mbili jirani Burundi ilichukua uamuzi kupunguza kiwango cha biashara na Rwanda. Wachambuzi wa mambo wanasema kuwa, kwa kutilia maanani muundo wa kijamii unaoshabihiana kati ya nchi mbili jirani za Burundi na Rwanda, kuna wasiwasi kuwa, iwapo mgogoro wa ndani nchini Burundi utapanuka na kushadidi zaidi yumkini ukaiathiri kwa kiwango kikubwa nchi jirani ya Rwanda. Jamii za nchi zote mbili za Rwanda na Burundi zinaundwa na watu wa makabila ya Hutu na Tutsi. 
Mivutano kati ya makabila hayo mawili ilipandikizwa na wakoloni na kushika kasi zaidi nchini Burundi katika kipindi cha kati ya mwaka 1993 na 2006. Wakati huo na baada ya kipindi cha miaka 25 ya utawala wa kabila la Tutsi, Burundi ilitawaliwa na mtu kutoka kabila la Hutu baada ya kushinda uchaguzi wa rais. Hata hivyo Melchior Ndadaye hakubakia madarakani muda mrefu na mauaji yake yalichochea zaidi machafuko na mapigano ya kikabila nchini humo.  
Kwa vyovyote vile kuongezeka mivutano ya kisiasa baina ya Rwanda na Burundi kunatishia amani na usalama wa eneo zima la Maziwa Makuu. Wakati huo huo inaonekana kuwa, safari za Rais Paul Kagame wa Rwanda katika nchi jirani za Kiafrika zinafanyika kwa shabaha ya kupata uungaji mkono wa viongozi wa nchi hizo katika mivutano ya Kigali na nchi kama Burundi na Ufaransa. Tarehe 10 mwezi uliopita wa Oktoba Rais Paul Kagame wa Rwanda alitishia kukata uhusiano wa nchi yake na Ufaransa. Sababu ya vitisho hivyo ni ripoti iliyotolewa na Kamisheni ya Kupambana na Mauaji ya Kimbari ya Rwanda ambayo iliwatuhumu maafisa wa ngazi za juu wa jeshi la Ufaransa kuwa walihusika katika mauaji hayo yaliyosababisha vifo vya karibu watu milioni moja wengi wao wakiwa wa kabila la Tutsi.  
Bunge la Burundi limepasisha sheria ya kujiondoa mahakama ya ICC
Katika upande mwingine wachambuzi wa mambo wamekosoa hatua ya Burundi ya kupunguza kiwango cha biashara kati ya nchi hiyo na Rwanda na vilevile uamuzi wa nchi hiyo wa kujiondoa katika Mahakama ya Kimataifa ya Jinai (ICC). Wachambuzi hao wanasema, hatua hiyo itaiathiri zaidi Burundi na kuifanya itengwe zaidi kisiasa na kiuchumi. Wanasema hatua kama hizo si za kimantiki hususan katika kipindi cha sasa ambapo Burundi inakabiliwa na mgogoro mkubwa wa kisiasa, ukosefu wa usalama na kutangatanga sehemu si ndogo ya raia hususan wa maeneo ya vijijini ambao ndio nguvu kazi kubwa katika sekta muhimu ya kilimo.   

No comments:

Post a Comment

Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages